Suratul Hijr ni Sura ya Makka. Nayo ina Aya 99. Imeanza kwa harufi za kutamkwa
zenye kueleza kwamba Qur'ani imejengeka kwa harufi hizi hizi mnazo zitumia katika
maneno yenu, na juu ya hivyo ni Muujiza kwenu, hamwezi kuleta kama hii. Kwani
aliye iteremsha ni Mwenyezi Mungu, Aliye takasaika, na Akatukuka. Na hizo harufi
pia ni kama kuwazindua wale wanao ipuuza Qur'ani, inawalingania, inawaita, waisikilize.
Asaa wakanufaika, na wakahidika kumfuata Mwenyezi Mungu.
Sura hii tukufu inabainisha ili watu wazingatie yaliyo wapata kaumu zilizo tangulia,
na khabari za Manabii walio kwisha pita, na yaliyo wapata kutokana na watu wao.
Na pia Sura hii inaonyesha ishara za Mwenyezi Mungu katika ulimwengu, katika mbingu
zilizo nyanyuliwa na zenye sayari ziilizo hifadhiwa, na ardhi iliyo tandikwa,
na kukunjuliwa, na milima iliyo simama imara, na pepo zenye kubeba maji, na zenye
kupandishia miti. Na Sura hii pia inaashiria mpambano wa mwanzo katika maumbile
ya asli baina ya maluuni Iblisi na Adam na mkewe, na kuendelea mpambano huo baina
ya kheri na shari mpaka imalizike dunia. Kisha tena malipo ya shari Siku ya Kiyama,
na malipo ya kheri. Na baada ya hayo Mwenyezi Mungu anasimulia visa vya Manabii
wawili, Ibrahim na Luut'i, na watu wa Al Hijr. Na Sura inaeleza cheo cha Qur'ani,
na hali ya washirikina katika kuipokea, na impasavyo Nabii kwa mnasaba wa ukafiri
wao, navyo ni kufikisha ujumbe wake, na kuutangaza, na kumuabudu Mwenyezi Mungu
mpaka ifike amri ya yakini.
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
1. Alif Lam Ra. (A.L.R). Hizi ni Aya za Kitabu na Qur'ani inayo bainisha. ***
2. HUENDA ikawa walio kufuru wakatamani wange kuwa Waislamu. ***
3. Waache wale, na wastarehe, na iwazuge tamaa. Watakuja jua. ***
4. Na hatukuuangamiza mji wowote ule ila ulikuwa na muda wake maalumu. ***
5. Hawawezi watu wowote kuitangulia ajali yao, wala kuchelewa. ***
6. Na walisema: Ewe uliyeteremshiwa Ukumbusho! Hakika wewe ni mwendawazimu. ***
7. Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli? ***
8. Sisi hatuwateremshi Malaika ila kwa sababu ya haki, na hapo hawatapewa muhula. ***
9. Hakika Sisi ndio tulio teremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutao ulinda. ***
10. Na hakika tulikwisha watumia Mitume mataifa ya mwanzo. ***
11. Na hakuwafikia Mtume ila walimkejeli. ***
12. Na kama hivi ndivyo tunavyo ingiza katika nyoyo za wakosefu. ***
13. Hawayaamini haya, na hali ya kuwa umekwisha wapitia mfano wa watu wa kale. ***
14. Na lau tungeli wafungulia mlango wa mbingu, wakawa wanapanda, ***
15. Basi wangeli sema: Macho yetu yamelevywa, bali sisi wenyewe tumerogwa. ***
16. Na hakika tumeweka katika mbingu vituo vya sayari, na tumezipamba kwa wenye
kuangalia. ***
17. Na tumezilinda na kila shetani afukuzwaye. ***
18. Isipo kuwa mwenye kusikiliza kwa kuibia, naye hufuatwa na kijinga cha moto
kinacho onekana. ***
19. Na ardhi tumeitandaza na humo tumeweka milima, na tumeotesha kila kitu kwa
kiasi chake. ***
20. Na tumekujaalieni humo vitu vya maisha yenu, na ya hao ambao nyinyi sio wenye
kuwaruzuku. ***
21. Na hakuna chochote ila asili yake inatokana na Sisi; wala hatukiteremshi
ila kwa kipimo maalumu. ***
22. Na tunazipeleka pepo za kupandishia, na tunateremsha kutoka mbinguni maji,
kisha tukakunywesheni maji hayo. Wala si nyinyi mnayo yaweka. ***
23. Na Sisi ndio tunao huisha na tunao fisha. Na Sisi ndio Warithi. ***
24. Na tunawajua walio tangulia katika nyinyi, na tunawajua walio taakhari. ***
25. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye atakaye wakusanya. Hakika Yeye ni Mwenye
hikima na Mjuzi. ***
26. Na tulimuumba mtu kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yaliyo
tiwa sura. ***
27. Na majini tuliwaumba kabla kwa moto wa upepo umoto. ***
28. Na Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Hakika Mimi nitamuumba mtu kwa
udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yaliyo tiwa sura. ***
29. Basi nitakapo mkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia. ***
30. Basi Malaika wote pamoja walimsujudia, ***
31. Isipo kuwa Iblisi. Yeye alikataa kuwa pamoja na walio sujudu. ***
32. (Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Iblisi! Una nini hata hukuwa pamoja na walio
sujudu? ***
33. Akasema: Haiwi mimi nimsujudie mtu uliye muumba kwa udongo unao toa sauti,
unao tokana na matope yenye sura. ***
34.(Mwenyezi Mungu) akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe ni maluuni! ***
35. Na hakika juu yako ipo laana mpaka Siku ya Malipo. ***
36. Akasema (Iblisi): Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watapo fufuliwa. ***
37. (Mwenyezi Mungu) akasema: Hakika wewe ni katika walio pewa muhula ***
38. Mpaka siku ya wakati maalumu. ***
39. Akasema: Mola wangu Mlezi! Ilivyo kuwa umenitia makosani, basi nahakikisha
nitawazaini hapa duniani na nitawapoteza wote, ***
40. Ila waja wako walio safika. ***
41. Akasema: Hii Njia ya kujia kwangu Iliyo Nyooka. ***
42. Hakika waja wangu, wewe hutakuwa na mamlaka juu yao, isipo kuwa wale wapotofu
walio kufuata. ***
43. Na bila shaka Jahannamu ndipo pahali pao walipo ahidiwa wote. ***
44. Ina milango saba; na kwa kila mlango iko sehemu walio tengewa. ***
45. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na chemchem. ***
46. (Wataambiwa:) Ingieni kwa salama na amani. ***
47. Na tutaondoa chuki iliyo kuwamo vifuani mwao, wawe ndugu juu ya viti vya
enzi wameelekeana. ***
48. Humo hayatawagusa machofu, wala hawatatolewa humo. ***
49. Waambie waja wangu ya kwamba Mimi ndiye Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. ***
50. Na kwamba adhabu yangu ndio adhabu iliyo chungu! ***
51. Na uwape khabari za wageni wa Ibrahim. ***
52. Walipo ingia kwake na wakasema: Salama! Yeye akasema: Hakika sisi tunakuogopeni. ***
53. Wakasema: Usiogope. Sisi tunakubashiria kijana mwenye ujuzi. ***
54. Akasema: Mnanibashiria nami uzee umenishika! Basi kwa njia gani mnanibashiria? ***
55. Wakasema: Tunakubashiria kwa haki; basi usiwe miongoni mwa wanao kata tamaa. ***
56. Akasema: Na nani anaye kata tamaa na rehema ya Mola wake Mlezi ila wale walio
potea? ***
57. Akasema: Hebu nini amri yenu, enyi wajumbe? ***
58. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa kaumu ya wakosefu! ***
59. Isipo kuwa walio mfuata Luut'i. Bila ya shaka sisi tutawaokoa hao wote. ***
60. Ila mkewe. Tunakadiria huyo atakuwa miongoni watao bakia nyuma. ***
61. Basi wale wajumbe walipo fika kwa Luut'i, ***
62. Alisema (Luut'i): Hakika nyinyi ni watu msio juulikana. ***
63. Wakasema: Bali sisi tumekuletea yale waliyo kuwa wakiyafanyia shaka. ***
64. Na tumefika kwako kwa Haki, na hakika sisi tunasema kweli. ***
65. Basi ondoka na ahli zako usiku ungalipo, nawe ufuate nyuma yao, wala yeyote
kati yenu asigeuke nyuma. Na mwende mnapo amrishwa. ***
66. Na tukamfunulia hukumu hiyo, ya kwamba hata wa mwisho wao hao ikifika asubuhi
atakuwa kesha katiliwa mbali. ***
67. Na wakaja watu wa mji ule nao furahani. ***
68. Akasema: Hakika hawa wageni wangu, basi msinifedheheshe. ***
69. Na mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi. ***
70. Wakasema: Sisi hatukukukataza usimkaribishe yeyote? ***
71. Akasema: Hawa binti zangu, ikiwa nyinyi ni watendaji. ***
72. Naapa kwa umri wako! Hakika hao walikuwa katika ulevi wao, wakihangaika ovyo. ***
73. Ukelele ukawatwaa wakipambaukiwa. ***
74. Na tukaigeuza nchi juu chini, na tukawanyeshea mvua ya mawe ya udongo wa
Motoni. ***
75. Hakika katika hayo zipo ishara kwa waaguzi. ***
76. Na miji hii ipo kwenye njia inayo pitiwa. ***
77. Hakika katika hayo ipo ishara kwa Waumini. ***
78. Na hakika watu wa Kichakani walikuwa wenye kudhulumu. ***
79. Kwa hivyo tukawaadhibu. Na nchi mbili hizi ziko kwenye njia ilio wazi. ***
80. Na bila ya shaka wakaazi wa Hijr waliwakanusha Mitume. ***
81. Na tuliwapa ishara zetu, nao wakazipuuza. ***
82. Nao walikuwa wakichonga majumba katika milima kwa amani. ***
83. Basi ukelele ukawatwaa asubuhi. ***
84. Hayakuwafaa waliyo kuwa wakiyachuma. ***
85. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake ila kwa ajili ya
Haki. Na hakika Kiyama kitafika. Basi samehe msamaha mzuri. ***
86. Hakika Mola wako Mlezi ndiye Muumbaji Mjuzi. ***
87. Na tumekupa Aya saba zinazo somwa mara kwa mara, na Qur'ani Tukufu. ***
88. Usivitumbulie macho yako vitu tulivyo waneemesha makundi fulani kati yao,
wala usiwahuzunikie. Na wainamishie bawa lako (la huruma) Waumini. ***
89. Na sema: Hakika mimi ni mwonyaji mwenye kubainisha. ***
90. Kama hivyo tuliwateremshia walio gawa, ***
91. Ambao wakaifanya Qur'ani vipande vipande. ***
92. Basi Naapa kwa Mola wako Mlezi! Tutawahoji wote, ***
93. Kwa waliyo kuwa wakiyatenda. ***
94. Basi wewe yatangaze uliyo amrishwa, na jitenge na washirikina. ***
95. Hakika Sisi tunatosha kukukinga na wanao kejeli. ***
96. Hao wanao fanya kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu yupo mungu mwingine. Basi,
watakuja jua! ***
97. Na Sisi tunajua kwa hakika kuwa wewe kifua chako kinaona dhiki kwa hayo wayasemayo. ***
98. Basi mtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi, na uwe miongoni wanao msujudia. ***
99. Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini. ***
Ukitaka kusoma Sura nyengine Rejea uliko toka
Ukiwa una shauri au maelezo juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com